Eti simpendi mke wangu kisa nilimshauri ang’olewe jino

Agosti 12 nilipata wasaa wakutembelea hospitalini kidogo, kama ujuavyo aendae hospitalini ni mgonjwa, basi, nilienda huko, kisa ili kuweza kujua hali yangu ya kiafya. Maana mara ya mwisho kutembelea hospitalini ni mwaka 1984 wakati wa sindano za ndui. Nilijongea KATIKA HOSPITALI MOJA ILIYOPO JIJINI Dar es Salaam na kuweza kufuata taratibu zote.
Lakini kabla ya kuanza safari, huko nyumbani kwangu, mke wangu nayeye alihitaji kwenda kwa tabibu kupata matibabu ya jino lake ambalo nalo lilikuwa likimsumbua kwa muda mrefu. Kama ujuavyo msomaji wa makala haya, dawa ya jino kung’oa! Kwa kuwa leo hii mzee wa kazi niliamua kwenda hospitali nayeye mama watoto wivu ukamjia.
Tulifanya safari ya kuelekea huko, unajua tena siye wazee wa madogo poromoka-pangu pakavu tia mchuzi, tulianza kwa kutembea mwendo wa dakika 20, tukapanda daladala kuelekea huko hosptalini na unajua tena lazima uzunguke na gari angalau abiria kuweza kukaa kwenye kiti.

Utaratibu wa Bima ya Afya
Tukiwa nyumbani, kila mmoja alibeba kitambulisho chake cha BIMA YA AFYA na kufuata utaratibu wa hospitali hiyo. Wajino akaenda kwa daktari wa meno na mie wa mguu nikaenda kwa dakitari wangu.

Mwezangu akaenda kwa wa meno akapata maelekezo juu ya kuzibwa kwa jino lake lililokuwa linamsumbua. Mwenzangu alimaliza mapema kupata huduma, madaktari wana mambo kweli kweli, yaliyofanyika huko ndani mie sijui ila nasema niliyosimuliwa tu. Kwa bahati nzuri nilikutwa sijaenda kumuona tabibu kulikuwa na foleni ndefu sana. Mamaa alinikuta na kuniuliza daktari wa ndani ni mwanamke au mwaname nikasema mie sijui.

Nikaingia kwa daktari na kukutana na tabibu mwanamke mrembo na daktari huyu aliniuliza kilichokuwa kinanisibu na nikapewa maelekezo ya cha kufanya ambapo niliambiwa nifanye vipimo na majibu nisiyachukue kwa siku hiyo, basi kwa kuwa nilikuwa mgonjwa mtiifu na nilifuata utaratibu wa daktari na kuelekea kwenye vipimo, mke wangu akiwa nyuma yangu

Basi nilifika nje ya mlango wa miale ya x na mhusika alianza kwa kuita majina ya wanaoingia humo, lilitajwa jina la kwanza, hakuna aliyeitika, la pili nalo vivyo hivyo na jina la tatu lilikuwa langu. Nikapewa maelekezo niingie chumbani, mwanadada aliliita jina langu kwa kulikatiza huku wagonjwa wengine wakidhani anayeitwa ni mwanamke. Kumbe ni mwanamme na tena baba wa watoto kadhaa.

Kwa nyuma yangu ikasikika minong’ono ”Huyu dada vipi mbona anamdhalilisha huyu baba kwanini kamuita Adela? Mke wangu akasema, jina lake ni Adeladius, huyu nesi amekatisha tu.” Mambo ya Ngoswe mwachie Ngoswe mwenyewe. Mie nikaingia ndani. Sikuweza kusema neno kwa kukatishwa jina langu akisema mkeo umesema wewe, kwa kuwa unapokuwa hospitali ni ulimwengu wa matabibu ukileta mchezo shauri yako, nilikuwa baba au kijana mtiifu sana. Nilipoingia ndani alikuja mama mmoja mrefu, akiuliza, wewe mbona unamuita mgonjwa mwingine na kumsahau mgonjwa wangu? Yule dada mhusika aliyeniita kwa kukosea jina langu akajibu kwa kunitazama mimi, eti kaka nimeita karibu mara ngapi hakuna aliyekuja? Mie nikajibu mama uliita mara tatu.

Basi nikaelekezwa cha kufanya na kupanda katika kitanda kikubwa cha chuma na kupigwa picha ya miale ya x na kuelekea hatua ya pili ya vipimo vya damu. Lakini kumbuka nilijulishwa na tabibu wangu kuwa majibu yatachukuliwa kesho saa saba mchana ili yaweze kufanyiwa tafsiri na wahusika.

Kweli mumeo anakupenda?
Nilitoka na kuanza safari ya kurudi kwetu madogo poromoka;Tukiwa njiani kila mmoja wetu anamuuliza mwezake hali ya matibabu. Mamaa akasema unajua nilipoenda kwa daktari nilitaka kwenda kung’oa jino maana lilikuwa linanisumbua sasa daktari kaniuuliza yani mumeo amekuruhusu kung’oa jino la mbele tena jino la kicheko, Kwelimumeo anakupenda? Maana hilo jino likitolewa tambua kuwa muonekana wako hautakuwa mzuri.

Lakini msomaji wa makala haya kupitia tovuti ya TBC mimi nilitoa ruhusa kwa kuwa mke wangu kwani alikuwa akilalamikia maumivu ya jino hilo kama nilivyokwambia hapo awali kuwa raha ya jino kung’oa

Basi tukafika nyumbani kwetu na kumbuka mie nilipewa maelekezo ya kumuona daktari wa kike siku inayofuata na mke wangu alipewa maelekezo ya kumuona daktari siku ya alhamisi. Kulipokucha niliamka mapema na kupitia kazini kupewa kibali cha kuelekea kwa tabibu ili kuchukua vipimo na kujua kipi kilikuwa kinanisumbua basi nilifika hospitali na kama kawaida mambo ya foleni nikaandikisha na kufuata majibu ya vipimo vyangu.

Ulimwengu wa Tekinolojia
Nikiwa hospitalini niligundua mengi hasa kuwa sasa ni ulimwengu wa tekinolojia kila linalofanyika linawekwa kwenye mtandao sasa hivi mafaili ya wagonjwa yanakuwa ya kimtandao na sio mafaili ya karatasi ya zama zile, nilimfuta tabibu na kupewa majibu ya vipimo vyangu na kupewa tiba huku daktari akitazama faili langu katika kompyuta yake.

Niliporudi nyumbani mamaa aliniuliza maswali mengi juu ya matibabu yangu na kubwa ni kwanini tabibu alinipangia niende kesho yake. Basi nilimwambia kuwa vipimo vyangu vilihitajika kufanyiwa tafsiri ndiyo maana niliambiwa kurudi kesho yake na nimepewa matibabu na ninamshukuru sana daktari huyo.

Yangu mie yalimalizika jana ila leo hii mke wangu anaenda kuziba jino lake kwa daktari yuleyule aliyemuuliza mke wangu kama kweli nampenda. Yeye ndiye ametoa ushauri wa jino la mke wangu kuzibwa badala ya kung’olewa, lakini mie ninaamini katika kuheshimu taaluma yoyote ile.

Kwa upande wangu nilipata dawa nzuri za daktari yule mrembo, kama unaleta wivu basi wewe hautaki kupona hospitalini, mie nataka kupona kama ilivyo kwa mke wangu. Ninachojilaumu ni kimoja tu nilisahau kuomba nambari ya simu ya daktari wangu angalau siku nyengine ningempigia simu kumueleza hali yangu inavyoendelea. Msomaji wa makala haya je nimechelewa kuiomba nambari ya simu ya tabibu huyu? Binafsi ninaamini sijachelewa nitaenda kumuomba nambari yake ya simu daktari wangu

Post a Comment

0 Comments