MTOTO ALBINO AKATWA KIGANJA JAMII AFANYE NINI

Mtoto Baraka aliyekatwa kiganja cha mkono wa kulia na watu wasiojulikana kijijini kwao juzi akiwa amelala kitandani akiendelea kupatiwa matibabu katika hospitali ya Rufaa Mbeya. 
Ni masikitiko makubwa kwamba mtoto mwenye ulemavu wa ngozi katika Kijiji cha Kipeta, Wilaya ya Sumbawanga mkoani Rukwa amejeruhiwa na watu wasiojulikana baada ya kukatwa kiganja cha mkono wa kulia.
Tukio hilo limekuja kipindi ambacho Serikali imeweka mikakati ya kupambana na wauaji wa albino nchi nzima. Pia, tukio hilo limekuja siku chache tu baada ya wananchi wenye ulemavu wa ngozi kumfikishia kilio chao Rais Jakaya Kikwete ambaye aliwaahidi kuwa serikali yake itahakikisha inawalinda na kuwatafuta watu wanaojihusisha na kukata viungo vyao au kuwaua.
Pamoja na hatua hiyo ya Rais Kikwete wiki iliyopita, watu wenye imani potofu za kishirikina mwishoni mwa wiki walimkata kiungo mtoto huyo baada ya kumpiga mama yake na kitu kizito hadi akazirai. Tunaambiwa kwamba alipozinduka alipiga kelele kuomba msaada kutoka kwa majirani. Hata hivyo, alipata msaada baada ya watu hao kukimbia, huku tayari wakiwa wametekeleza uovu wao. Kama wananchi wengi wanavyofahamu, huo ulikuwa ni mwendelezo wa matukio mengi kama hayo dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi, yaani albino.
Tumepata faraja kusikia kwamba Serikali tayari imewakamata washukiwa kadhaa wa tukio hilo sawa na wale waliofanya uovu kama huo mwezi uliopita katika Kijiji cha Shilabela, mkoani Geita ambako watu kadhaa walivamia nyumba ya mama mmoja na kumpora mtoto wake albino, huku wakimjeruhi vibaya mama huyo alipokuwa akipambana nao kujaribu kumwokoa mwanaye.
Tunaweza kuorodhesha matukio mengi ya albino kuuawa au kujeruhiwa, lakini tunadhani kwamba pengine wakati umefika sasa kwa jamii kuelekeza nguvu zake katika kukomesha imani hizo potofu, kwani ni dhahiri kwamba sheria kali pekee zimeshindwa kukomesha vitendo hivyo vya kinyama dhidi ya albino.
Hakuna sababu za kisayansi zinazotolewa kuhusu kazi za viungo vya albino, ingawa kila likifanyika tukio la aina hiyo, jamii huambiwa ni kwa shughuli za ushirikina; kwamba watu wanaotafuta utajiri kwa njia za mkato ndio wanaohusika.
Kwamba waganga wa kienyeji ambao hufanya shughuli zao kwa kupiga ramli ndio huwaagiza wateja wao kupeleka viungo vya albino ili watengenezewe mambo yao. Ni kutokana na hali hiyo Serikali imeamua kupiga marufuku upigaji ramli na katika maeneo mengine nchini wapigaji ramli wamekamatwa ili wachukuliwe hatua za kisheria.
Tunaipongeza Serikali kwa hatua hiyo, lakini tunadhani iko haja kwake na jamii kwa jumla kushughulikia watu wanaokwenda kwa wapiga ramli wakijidanganya kwamba watatajirika au kupata vyeo kwa imani hizo potofu. Ni bahati mbaya kwamba baadhi ya wanasiasa ambao wanapaswa kuwa mstari wa mbele kupiga vita upigaji ramli unaodaiwa kuwa chanzo cha mauaji ya albino ndio wanaokwenda kupiga ramli na huenda ndio wanaowatuma wengine kufanya hivyo kwa malipo kidogo.
Katika mapambano dhidi ya ushirikina ni vyema Serikali, asasi za kiraia na jamii kwa jumla vikatoa elimu ili kila mwananchi atambue kwamba siri ya utajiri ni kufanya kazi kwa juhudi na weledi ofisini, mashambani, migodini na kwingineko. Vilevile, watu wapewe elimu ya kujitegemea kuhusu namna ya kupata mitaji, kuweka kumbukumbu na kujiepusha kufanya anasa na matumizi yasiyo na maana. Hiyo ndiyo siri pekee ya mafanikio na wala siyo viungo vya albino.

Post a Comment

0 Comments