Michezo Vikao, mikwara, vitisho vimeiua Yanga

Wachezaji wa timu ya Yanga wakimsihi Haruna Niyonzima atoke uwanjani baada ya kupewa kadi nyekundu
Kwa ufupi
Jambo linalochangia Yanga kuwa na wakati mgumu katika mechi dhidi ya Simba ni kwamba wanakuwa katika presha kubwa ya mchezo kuliko Simba.
Dar es Salaam.Vikao virefu, vitisho vya wazee pamoja na baadhi ya viongozi wakiwatuhumu wachezaji sita kuhujumu timu hiyo vimetwaja kuwa ni sababu ya Yanga kufungwa na Simba juzi kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Yanga ilifungwa na Simba bao 1-0 juzi, shukrani kwa bao la Emmanuel Okwi alilolifunga kwa shuti la umbali wa mita 35 na kuwazima mashabiki wa Yanga waliofurika uwanjani hapo wakiamini watashinda mchezo huo.
Taarifa kutoka ndani ya Yanga zinasema kwamba siku mbili kabla ya mchezo wazee wa klabu hiyo walitua kambini usiku na kuzungumza na wachezaji hadi usiku wa manane, huku wakiwachimba mikwara iliyochangia kuwatisha baadhi ya wachezaji na kuwatoa mchezoni.
Chanzo hicho kilisema wazee hao waliwaambia wachezaji wao kuwa wanasikia kuna baadhi wamehujumu mechi hiyo hivyo wanatakiwa kuwa makini kwani wamechoshwa na mashabiki wao kufa kwa presha uwanjani kutokana na matokeo mabaya wanayopata kutoka kwa Simba.
“Yaani wachezaji walipigwa mkwara kabla ya mchezo ule na wazee wa klabu ambao walikwenda kuzungumza na wachezaji Ijumaa usiku na walionekana kabisa wamepania kwani walionekana wanaongea kwa jazba na wachezaji wengi waliingiwa na hofu,”kilisema chanzo chetu hicho cha habari.
Wachezaji waliodaiwa kuhujumu timu hiyo kwa kucheza chini ya kiwango ni pamoja na kipa Ali Mustapha ‘Barthez’, Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Amissi Tambwe, Danny Mrwanda pamoja na Kelvin Yondani.
Hata hivyo, Mustapha’Barthez’ alikuwa kwenye wakati mgumu zaidi akitakiwa kuwa makini golini na asifungwe mabao ya kizembe kama alivyofanya kwenye mechi ya ligi msimu uliopita iliyomalizika kwa sare ya 3- 3.
Barthez juzi alifungwa bao la umbali wa mita 35 na Okwi, lililosababisha baadhi ya mashabiki kumtafuta kwa lengo la kumpiga, lakini Polisi walimuokoa na kumuingiza kwenya basi la wachezaji na kulisindikiza hadi lilipoondoka.
Baada ya kipenga cha mwisho cha mwamuzi Martin Saanya, kipa huyo alimwaga machozi na aliendelea kulia hata alipoingia katika vyumba vya kubadilishia nguo na hivyo kuwapa kazi wachezaji wenzake kumbembeleza.
Wachambuzi wanena
Wachambuzi wa masuala ya soka nchini wamesema kufungwa kwa Yanga kumechangiwa na kocha Hans Pluijm kwanza kuchezesha nusu ya kikosi chake washambuliaji, pili kuwa na wachezaji wenye umri mkubwa na tatu wachezaji kuathirika kisaikolojia.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tofauti jana, wachambuzi hao, Edo Kumwembe na Kenny Mwaisabula walisema, wachezaji wenye umri mkubwa na kitendo cha kufungwa mara kwa mara na Simba na mfumo wa timu uliotumiwa na Pluijm ndivyo vilizamisha jahazi la Yanga huku kipa Ally Mustafa ‘Barthez’ akikingiwa kifua kwa bao alilofungwa.

Post a Comment

0 Comments