LOWASSA RAIS 2015

SASA ni wazi kuwa waziri mkuu wa zamani, Edward Ngoyai Lowassa ndiye atakuwa rais wa awamu ya tano Tanzania mwaka 2015, kutokana na ukweli kwamba kambi zinazosigana ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), zinaonekana kupwaya huku yake ikiwa na watu wenye nguvu kisiasa na kiuchumi, Risasi Jumamosi linakuwa la kwanza kusema.
Katika vuguvugu la nani awe rais mwaka 2015, uchunguzi wa gazeti hili ulionesha kuwa tangu uchaguzi ndani ya chama hicho mwaka jana, Lowassa anaonekana kupata mafanikio zaidi kisiasa, ikilinganishwa na mahasimu wake, Benard Membe na Samuel Sitta ambao wanatajwa kutaka kuwania urais baada ya Dk. Jakaya Mrisho Kikwete kumaliza muda wake.
Kama ilivyo kwa Lowassa, Sitta ambaye ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Membe mwenye kofia ya Uwaziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, nao wamekuwa wakidaiwa kuwa na makundi katika harakati za kuusaka urais, japokuwa wenyewe hawajathibitisha.
Uchunguzi huo umeonesha kuwa Lowassa ana mtandao wenye nguvu kisiasa na wachunguzi wa mambo wanasema hata kama vikao vya juu vitamkata jina, kundi lake likiamua nani awe rais uwezekano wa mtu huyo kupita ni mkubwa.
Katika uchaguzi wa chama katika mikoa, wafuasi wengi wa Lowassa walipeta ukilinganisha na makundi mengine yanayotajwa katika kinyang’anyiro cha urais.
Baadhi ya wasomi nchini, walitofautiana kimtazamo kuhusu chaguzi hizo ndani ya CCM. Mhadhiri maarufu wa UDSM, Dk. Benson Bana alisema CCM katika chaguzi hizo imeonesha kwamba hakuna kiongozi yeyote mwenye hati miliki ya chama hicho kwani mtu yeyote anaweza kuingia na kuondoka kwenye chama hicho.
Naye Kisena Mabuba ambaye ni Mhadhiri katika Chuo cha Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere alisema: “Tofauti na matarajio ya wengi kuwa CCM ingemeguka, mimi ninachokiona hapa kundi lililobaki na nguvu ni lile la mwenyekiti mwenyewe. Kundi moja limefutwa kabisa na mengine yameshindwa kupata nguvu za kutosha.”

Post a Comment

0 Comments